facebook likes

Monday, August 12, 2013

WACHEZAJI WAPYA WA SIMBA KAZE GILBERT NA KHAMIS TAMBWE WAZUIWA NCHINI BURUNDI..!!

NYOTA wapya wawili wa Klabu ya Simba, straika Khamis Tambwe na beki Kaze Gilbert, watachelewa kujiunga na timu hiyo baada ya klabu yao ya Vital’O ya Burundi kuwazuia kwa muda.

....SOMA ZAIDI.....

Nyota hao tangu waliposaini mikataba Msimbazi na kurejea kwao hawajarudi na juzi hawakuonekana katika Tamasha la Simba Day kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, licha ya Simba kuwa na utaratibu wa kulitumia kwa ajili ya kuwatambulisha wachezaji wake wote kabla ya msimu kuanza.

Awali, wachezaji hao walitarajiwa kutua nchini mwishoni mwa wiki iliyopita, lakini haikuwa hivyo, hali iliyowalazimu Simba kuanza kuwafuatilia kwa haraka.

Joseph Itang’are, ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Simba, ameliambia Championi Jumatatu kuwa, nyota hao wameshindwa kuwasili kwa wakati, baada ya klabu yao kuwazuia kwa muda, ikitaka wamalizie michezo iliyobaki ya Ligi Kuu ya Burundi kabla haijaachana nao rasmi.

Itang’are, maarufu kama Mzee Kinesi, alisema vital’O ilikuwa imebakiza michezo miwili, mmoja ukichezwa juzi.

Mzee Kinesi alisema Vital’O imepanga kuwapa baraka za kuja Tanzania katikati ya wiki hii, tayari kwa kuanza maisha mapya na Wekundu hao.

Tulilazimika kuwasiliana nao haraka baada ya kuona kimya, lakini hata klabu yao nayo imeonyesha uungwana wa kutupigia na kutueleza kuwa wachezaji hao ni muhimu sana kwao wakati huu ligi yao ikielekea ukingoni,” alisema Mzee Kinesi.

“Kwa shingo upande ilibidi tuwakubalie kwa kuwa sisi bado hatujaanza ligi ya huku kwetu, ingawa tunajua kuchelewa kwao kunaweza kumchelewesha kocha wetu kutengeneza kikosi chake, tunaamini mpaka kufikia katikati ya wiki ijayo (wiki hii), watakuwa wameshafika nchini.”

Nyota hao wanatarajiwa kuongeza nguvu katika kikosi cha Simba. Tambwe alikuwa mfungaji bora kwenye michuano ya Kombe la Kagame iliyomalizika hivi karibuni nchini Sudan, wakati Kaze alikuwa mhimili mkubwa katika kikosi chao cha Vital’O kilichotwaa ubingwa wa michuano hiyo.

No comments:

COMMENTS

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...