facebook likes

Monday, August 12, 2013

DK MWAKYEMBE: WANASIASA WANAKUZA MGOGORO WA MPAKA ZIWA NYASA


Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, amewatolea uvivu wanasiasa na kuwaambia wao ndiyo wanaokuza suala la mgogoro wa mpaka wa Ziwa Nyasa kati ya Tanzania na Malawi.
....SOMA ZAIDI......
Dk. Mwakyembe alitoa kauli hiyo jana baada ya kutembelea bandari ya Kiwira iliyopo wilayani Kyela kukagua shughuli za ujenzi na kukuta meli kubwa ya mizigo ijulikanayo kama Katundu mali ya serikali ya Malawi ikiwa imetia nanga katika ardhi ya Tanzania ikipakia shehena ya mbolea katika bandari hiyo.
Dk. Mwakyembe alisema toka zamani watumiaji wa ziwa hilo wanafahamu kwamba ukifika eneo fulani ndani ya ziwa hilo unakuwa eneo la Tanzania au Malawi na hivyo chombo husika kikifika katika nchi husika kinalazimika kupeperusha bendera ya nchi hiyo. Alisema haiingii akilini kama wanasiasa wanawapotosha wananchi wa nchi hizo kwa manufaa yao binafsi kwani suala la mgogoro wa mpaka huo halijaathiri sekta ya usafirishaji.
 
Akizungumza na wafanyakazi wa bandari hiyo, aliwahakikishia watumiaji wa Ziwa Nyasa kuwa sekta ya usafirishaji haijakumbwa na tofauti hizo za mipaka ndani ya ziwa hilo na hivyo shughuli za usafirishaji zinaendelea kama kawaida.
Kwa upande wake nahodha wa meli ya Katundu, Kapteni Mponda alipongeza juhudi zinazofanywa na serikali ya Tanzania kujenga bandari ya Kiwira ambayo inakuwa bandari ya pili kubwa kwa upande wa Tanzania ikiwemo bandari ya Itunge.
 
Mgogoro wa mpaka kati ya Malawi na Tanzania umedumu kwa muda mrefu hivi sasa unasuluhishwa na marais wastaafu, Joachim Chisano wa Msumbiji na Thabo Mbeki wa Afrika Kusini.
 
Mwezi uliopita, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, alisema marais hao wastaafu walienda Malawi kukutana na Rais Joyce Banda.

No comments:

COMMENTS

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...