facebook likes

Saturday, August 3, 2013

TANZANIA YAREJESHA KWAO WAKIMBIZI LAKI SITA NA KUFUNGA KAMBI 12 ZA WAKIMBIZI

Dk. Emmanuel Nchimbi Waziri wa mambo ya ndani
dk emmanuel nchimbi
Serikali ya Tanzania imewarejesha kwao kwa hiari wakimbizi wapatao569,018 toka nchi za Maziwa Makuu waliokuwa wamehifadhiwa hapa nchini kutokana na machafuko katika nchi zao.  Kati ya hao 502,358 walitoka nchini Burundi na 66,660, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.  Wakimbizi hawa wamerejeshwa kwao kufuatia zoezi lililoanzishwa rasmi mwaka 2002 kwa wakimbizi toka Burundi na mwaka 2005 kwa wakimbizi toka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRS), baada ya usalama katika nchi zao kuimarika.
Sambamba na mafanikio haya, pia kambi 12 kati ya 13 zilizokuwa zikitumika kuwahifadhi wakimbizi hawa zimefungwa, na hadi sasa ni kambi moja tu ya wakimbizi ya Nyurugusu, wilayani Kasulu mkoani Kigoma ndiyo iliyobakia ikiwahifadhi wakimbizi kutoka DRC (63,728), Burundi (4,153) na nchi nyingine mchanganyiko za Kiafrika (212).
Tanzania inajulikana kimataifa kama nchi mojawapo ambayo imechangia kwa kiasi kikubwa kutoa hifadhi kwa wakimbizi wanaokimbia nchi zao kutokana na machafuko ya kiaiasa ambapo mwaka 1995 idadi yao ilifikia zaidi ya milioni moja.
Lengo la Serikali ni kuona kuwa suala la kuhifadhi wakimbizi hapa nchini linafikia ukomo na juhudi zinaendelea kuona kuwa hata Kambi ya Nyarugusu ambayo ndiyo kambi pekee iliyobakia inafungwa baada ya wakimbizi walio katika kambi hiyo kurejeshwa kwao, pale hali ya usalama nchini DRC itakapokuwa imeimarika.
Kuondoka kwa wakimbizi hawa sasa kunatoa nafasi kwa Serikali na wananchi kutumia kwa shughuli nyingine za kimaendeleo maeneo makubwa yaliyokuwa yanatumika kuhifadhi wakimbizi, lakini pia kunatoa nafasi nzuri ya kuweza kukabiliana na changamoto za kiusalama katika maeneo hayo ambayo yapo katika mikoa ya mpakani mwa nchi.
Serikali inapenda kuishukuru Jumuiya ya Kimataifa kupitia Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), kwa misaada ya hali na mali waliyotoa na wanayoendelea kutoa kusaidia hifadhi ya wakimbizi hapa nchini. Pia Watanzani wote na hasa wale wa mikoa ya Katavi, Kigoma na Kagera kwa ushirikiano waliotoa kwa wakimbizi waliokuwa wamehifadhiwa katika maeneo yao, na nchi za Burundi, Congo kwa ushirikiano wao uliowezesha kuwarejesha raia wao waliokuwa wamehifadhiwa hapa nchini.
Mashirika mengine ambayo pia yalihusika na yanaendelea kutoa huduma za kibinadamu kwa wakimbizi ni pamoja na Shirika la Chakula Duniani (WFP), Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Kuhudumia Watoto (UNICEF), Kamati ya Kimataifa ya Uokozi (IRC), na Shirila la Msalaba Mwekundu Tanzania (TRCS).
Imeandaliwa na Felix Mwagara
KITENGO CHA MAWASILIANO YA SERIKALI
WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI

No comments:

COMMENTS

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...