facebook likes

Friday, July 5, 2013

JAJI MKUU WA MAHAKAMA YA KIKATIBA KUIONGOZA MISRI

Rais wa Misri aliyeondolewa madarakani, Mohammed Morsi.
Jaji Mkuu wa Mahakama ya Kikatiba nchini Misri, Adli Mansour anatarajiwa kuapishwa kama rais wa mpito wa nchi hiyo baada ya jeshi kumng'oa madarakani rais Mohammed Morsi, ambaye ni kiongozi wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia nchini humo.
Mkuu wa Jeshi, Generali Abdul Fattah al-Sisi alitoa tangazo hilo kupitia televisheni Jumatano jioni.

Baadhi ya waandamanaji waliokuwa wakimpinga rais Morsi.
Generali Sisi alisema kuwa Morsi, ambaye ni rais wa kwanza kuchaguliwa amekosa kutimiza mahitaji ya watu.
Hatua hiyo inakuja baada ya siku nyingi za maandamano dhidi ya rais Morsi wa chama cha Muslim Brotherhood.
Waandamanaji walimtuhumu yeye na chama chake kwa kusukuma ajenda ya Kiislamu kwa taifa hilo na kukosa kusuluhisha matatizo ya kiuchumi yanayolikumba taifa hilo.

Chama cha Muslim Brotherhood kimesema kuwa bwana Morsi pamoja na washauri wake wako chini ya kifungo cha ndani na hawana mawasiliano ya nje.
Hapo awali, Mkuu wa Majeshi alisema kuwa jaji mkuu wa taifa hilo atachukuwa mamlaka ya rais.
Maelfu ya waandamanaji wanaompinga bwana Morsi mjini Cairo walisherehekea kwa shangwe na vifijo kufuatia taarifa hiyo ya jeshi lakini wale wanaomuunga mkono bwana wanasemekana kubaki kimya huku wakisubiri matukio yatakayofuata.

Rais Obama amesema kuwa ana wasiwasi mkubwa kuhusiana na matukio yaliyopo nchini Misri huku Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Banki Moon akitaka kuwe na utulivu.
(Habari: BBC Swahili)

No comments:

COMMENTS

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...