facebook likes

Thursday, August 1, 2013

HATIMAYE MUDA WA SAA 48 ZA KUSALIMISHA SILAHA KWA WAASI WA M23 UMEMALIZIKA-WAKATI WOWOTE MAPIGANO YANAWEZA ANZA




New York. Muda wa saa 48 wa kusalimisha silaha kwa waasi wa March 23(M23), Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo umemalizika na wakati wowote mapigano yanaweza kuanza.
Misheni ya Kutuliza Amani ya Umoja wa Mataifa(Monusco) , ilitoa saa hizo zinazomalizika leo na Jeshi la UN litaanza kutumia nguvu kunyang’anya silaha waasi hao.
Taarifa iliyotolewa na Monusco iliyotolewa na Msimamizi wa Misheni hiyo, Luteni Jenerali Carlos Alberto dos Santos Cruz na kusambazwa na Idara ya Mawasiliano ya Umoja wa Mataifa jana, inaeleza kwamba, watu binafsi katika eneo la Kivu ya Magharibi ambalo linajumisha Goma na Sake na ambao hawahusiki na vyombo vya usalama wamepewa saa 48 kuanzia saa kumi jana (juzi) kwa saa za Goma (Jumanne) kuzisalimisha silaha zao.
Taarifa ilisema, “Baada ya saa 10 jioni ya Alhamisi, Agosti Mosi, wale wote ambao watakuwa hawajasalimisha silaha zao watachukuliwa kama tishio kwa usalama wa wananchi na Monusco itachukua hatua zote muhimu kuwapokonya silaha hizo ikiwa ni pamoja na kutumia nguvu kama ilivyoainishwa katika mamlaka na sheria za ushiriki za Monusco.”
Kwa mujibu wa taarifa hiyo zaidi ya wananchi milioni moja wanaishi katika eneo dogo la Goma na Sake na kandokando ya barabara ambayo inawaunganisha na kambi ya wakimbizi ya Mugungu ambayo ni makazi ya muda ya watu karibu 70,000 ambao wameyakimbia makazi yao kutokana na mapigano.
Kwa mujibu wa Monusco,tangu katikati ya Mei eneo hilo limeshuhudia mapigano ya mara kwa mara kutoka kwa Kundi la M23 dhidi ya Majeshi ya Serikali ya FARDC ikiwa ni jaribio la wazi la kutaka kusonga mbele kuelekea Goma na Sake. “Katika mashambulizi hayo,likiwamo la hivi karibuni la Julai 14, M23 walitumia kiholela silaha zao za moto zikiwamo silaha nzito ambazo zimesababisha wananchi kujeruhiwa.”
Taarifa hiyo imeongeza kwamba kundi hilo la M23 katika mashambulizi hayo limelenga pia Vituo vya Umoja wa Mataifa.
Taarifa hiyo inabainisha kwamba eneo hilo maalumu la usalama (security zone)litasaidia kudhibiti tishio la moja kwa moja mbali na eneo la nje ya Goma na pengine eneo hilo linaweza kupanuliwa na kurudiwa sehemu nyingine kutakako hitajika.
Tamko hilo la kutoa saa 48 kwa waasi kusalimisha silaha zao linafuatia kuwasili katika eneo la Goma kwa Kamanda Mkuu wa Monusco, Luteni Jenerali Carlos Alberto dos Santos Cruz ambaye alitangaza kwamba Misheni ya Monusco itaunga mkono Jeshi la Serikali(FARDC) katika kuanzisha eneo la usalama kuzunguma eneo la Goma na vitongoji vyake.

No comments:

COMMENTS

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...