facebook likes

Wednesday, October 9, 2013

Wanasoka wanaojirusha na watoto wa mabosi wao

Staa huyu wa kimataifa wa Brazil hakuogopa kugonga mlango wa nyumba ya bosi wake mmiliki wa klabu ya AC Milan ambaye pia ni Waziri Mkuu wa Italia, Silvio Berlusconi na kuomba namba ya simu ya binti yake, Barbara Berlusconi ambaye pia ni mmoja kati ya wanabodi wa AC Milan. 
SOMA ZAIDI.....
LONDON, ENGLAND
WAKATI mshambuliaji wa Manchester United, Wilfried Zaha, akiwa ameingia matatani kutokana na uvumi ulionea katika mitandao ya kijamii akidaiwa kutembea na binti wa kocha wake, David Moyes, imegundulika kuwa hata kama amefanya kitendo hicho, Zaha hawezi kuwa mchezaji wa kwanza kulala na mtoto wa kocha wake. Wapo wengi tu.
Sergio Aguero
Katika muunganiko ambao ni kama ulipangwa makusudi kwa ajili ya kumleta mwanasoka aliyekamilika zaidi duniani, nyota huyo wa Manchester City aliamua kutoka kimapenzi na Giannina Maradona, mtoto wa Diego Maradona ambaye ni kocha wake wa zamani katika kikosi cha Argentina kilichoriki Kombe la Dunia mwaka 2010 nchini Afrika Kusini.
Februari mwaka 2009 walipata mtoto wa kiume aitwaye Benjamin. Mtoto huyo alipelekwa kutazama mechi yake ya kwanza ya soka akiwa na umri wa wiki mbili.  Ilikuwa katika pambano baina ya Atletico Madrid dhidi ya Barcelona. Baba yake alifunga mabao mawili ya timu yake.
Stan Collymore
Mbabe wa zamani wa Liverpool. Yeye alitumia kitabu cha maisha yake ya soka kufichua siri kwamba aliwahi kufanya ngono kwa usiku mmoja na Stacey ambaye ni mtoto wa kocha wake wa zamani, Roy Evans. Anasema ilikuwa ni katika usiku ambao Liverpool ilichapwa bao 1-0 na Manchester United katika fainali za Kombe la FA.
“Sikutaka kwenda huko. Si kwa sababu sikumpenda, hapana, ni kwa sababu Roy na mkewe walikuwa watu wazuri sana. Hata hivyo nilikwenda na tukafanya ngono katika chumba cha hoteli  kilichofuatana na walicholala wazazi wake,” anasimulia Collymore ambaye ni mmoja kati ya wachezaji mahiri kuwahi kutokea katika historia ya Liverpool. Enzi zake alikuwa anaaminiwa mno na Evans.
Ronaldinho Gaucho
Unaweza kuiweka orodha hii bila ya jina la mmoja kati ya wachezaji wapenda vimwana kama Ronaldinho? Kwa mujibu wa gazeti maarufu la michezo la Hispania, Ronaldinho aliwahi kutoka kimapenzi na mtoto wa kocha wake wa zamani katika kikosi cha Barcelona, Lindsay Rijkaard.
Inasemekana Rijakaard hakufurahishwa na uhusiano huu kutokana na tabia za uhuni za Ronaldinho ambaye alisifika kwa kutembelea klabu nyingi za usiku za Barcelona akiwa na vimwana mbalimbali karibu yake.
Van Bommel
Ni kiungo wa zamani wa Barcelona, AC Milan na timu ya taifa ya Uholanzi. Yeye aliamua kumchukua jumla kabisa mtoto wa kocha wake, Bert van Marwijk, anayejulikana kwa jina la Andra.
Wawili hao wana watoto watatu ambao ni Thomas, Ruben na Renee. Van Bommel alikuwa katika kikosi cha Uholanzi kilichoshiriki Kombe la Dunia nchini Afrika Kusini huku kocha wake mkuu akiwa Van Marwijk.
Wakati Fulani, kocha huyo aliwahi kushutumiwa kwa kumtupa nje ya kikosi kiungo, Nigel Di Jong, na kumpanga Van Bommel huku mashabiki wakihisi kuwa ulikuwa ni upendeleo kwa mkwe wake.
Paul Peschisolido
Nyota huyu raia wa Canada alitoa kali ya mwaka baada ya kuamua kufunga kazi kwa kumuoa bosi wake klabuni. Peschisolido alitoka kimapenzi na bosi mkuu wa klabu ya Birmingham City, Karren Brady, katika msimu wake wa kwanza kama mshambuliaji wa timu hiyo mwaka 1995.
Baadaye walioana na kupata mtoto mmoja aliyeitwa Sophia. Akijitetea kuhusu uhusiano huo, Peschisolido alisema: “Haikuwekwa katika mkataba wangu kwamba nisifanye hivyo.”
Mauricio Caranta
Ni kipa mahiri wa Boca Juniors ya Argentina.
Huyu alikiona cha mtema kuni baada ya kufukuzwa mazoezini, kuondolewa katika timu na kutishiwa kuuzwa katika dirisha la uhamisho baada ya kutoleana maneno makali na kocha wake, Carlos Ischia.
Uvumi ulikuwa umesambaa kwamba staa huyo alikuwa amelala na mtoto wa Ischia na ndio kisa cha ugomvi wao. Hata hivyo, Caranta alijitetea kwamba hajafanya hivyo na mpaka sasa haieleweki kama ni kweli alifanya hivyo au hapana.
Alexander Pato
Staa huyu wa kimataifa wa Brazil hakuogopa kugonga mlango wa nyumba ya bosi wake mmiliki wa klabu ya AC Milan ambaye pia ni Waziri Mkuu wa Italia, Silvio Berlusconi na kuomba namba ya simu ya binti yake, Barbara Berlusconi ambaye pia ni mmoja kati ya wanabodi wa AC Milan.
Barbara alilitetea hadharani penzi lake na Pato ambaye kwa sasa amerudi kwao Brazil kucheza soka akisaka nafasi ya kucheza Kombe la Dunia.
“Najiona kama msichana mdogo ambaye amempenda mwanaume aliyevutiwa naye. Sioni kama nimevunja kanuni yoyote. Wote sisi ni vijana,” alisema Barbara.
“Uhusiano huu si ujinga. Nisingekuwa naye kama ningekuwa simpendi. Alexandre ni mtu ambaye ni mzuri sana katika kuchangia naye mambo mbalimbali.”
Hata hivyo, pamoja na Barbara kuwa mmoja kati ya wamiliki wa AC Milan, lakini bado hakuweza kuzuia Pato asirudi kwao Brazil kwenda kukipiga katika klabu ya Corinthians kutokana na kusugua benchi mara kwa mara katika kikosi cha AC Milan.

No comments:

COMMENTS

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...