facebook likes

Monday, September 9, 2013

Kibano chamgeukia Ndugai

*Yadaiwa alipewa maelekezo kuwabana wapinzani
*Profesa Lipumba adai uwezo wake bungeni mdogo
NAIBU Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai, amezidi kujiweka katika wakati mgumu, baada ya viongozi wa vyama vya upinzani kudai alipewa maelekezo na Serikali kupitisha Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Katiba.
SOMA ZAIDI..........
Kwa nyakati tofauti jana, viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Chama cha Wananchi (CUF), walisema ni wazi, Ndugai ameonekana kuwa na uwezo mdogo wa kuongoza Bunge, kutokana na kusababisha vurugu kubwa ndani ya ukumbi wa Bunge wiki iliyopita.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, alisema uwezo wa Ndugai kuongoza Bunge unahatarisha amani, mshikamano na umoja wa kitaifa uliopo sasa kutokana na kutokuwa na mtazamo mpana wa kufikiri.

Alisema mbali ya uwezo, kulikuwa na ajenda ya chini chini kati ya kiti cha Spika, Serikali na wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuhujumu malengo na nia ya Rais Jakaya Kikwete kuwa na Katiba Mpya ifikapo mwaka 2015.

Alisema kitendo cha Ndugai kuamuru polisi kumtoa ndani ya Bunge Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, ni cha aibu na cha kidikteta.

Alisema kuna baadhi ya viongozi wa Serikali (hakuwataja), wanajionyesha wanamsaidia Rais Kikwete lakini ndani ya mioyo yao wana ajenda za siri za kumhujumu.

Alisema viongozi hao wamekuwa wakitumia udhaifu wa Ndugai kwa kumshawishi kufanya kile wanachoona kinafaa, kwa lengo la kukandamiza upinzani na kumhujumu Rais Kikwete bila yeye kujua.

Alisema kuna kawaida kwa kiti cha Spika hasa kinapokaliwa na Ndugai kuendesha Bunge kwa kuipendelea Serikali kwa kadri kinavyoweza, huku kikizima hoja za upinzani kwa makusudi.

“Kuna njama za wazi zinafanywa na kiti cha Spika kwa kutelekeza maoni ya wananchi na kupendelea ya CCM, kwa upande wa Zanzibar hawakushirikishwa vizuri na hata wabunge wa CUF wanasema hawakushirikishwa.

“Moja ya njama za wazi ni ile ya wabunge 166 wa Bunge la Katiba wanaopaswa kupendekezwa na taasisi mbalimbali na kuteuliwa na rais, sisi CUF tunasikitishwa na mchakato unavyoendeshwa na jinsi uteuzi unavyopendekezwa.

“Hii Katiba Mpya itakuwa ni ya CCM si ya Watanzania, na ombi la wabunge wa CUF ni kutaka muswada urudishwe kwa wananchi na kamati ijadili upya,” alisema Profesa Lipumba.

Chanzo: Mtanzania 

No comments:

COMMENTS

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...