facebook likes

Tuesday, October 15, 2013

RAILA ODINGA AELEZA NYERERE ALIVYOMSAIDIA KUSOMA NJE

Waziri Mkuu wa zamani wa Kenya, Raila Odinga ameeleza kuwa bila ya Pasipoti ya Tanzania aliyopewa kwa msaada na Mwalimu Julius Nyerere asingeweza kwenda Ujerumani kusoma baada ya Idara ya Uhamiaji ya Kenya kumnyima hati hiyo ya kusafiria.
SOMA ZAIDI........
Odinga ambaye hivi sasa ni kiongozi mkuu wa Muungano wa Cord ameeleza hayo katika kitabu chake kiitwacho The Flame of Freedom, ambamo ameelezea historia yake na familia yake katika mambo mbalimbali.
Idara ya Uhamiaji ya Kenya ilimnyima Odinga hati hiyo kutokana na Serikali ya kikoloni kuzuia hati ya baba yake, mzee Jaramogi Odinga kwa sababu alitembelea nchi za Urusi na China zilizokuwa maasimu wakubwa wa nchi za Magharibi.(A.M)

Hata hivyo, Mzee Jaramongi aliamua kusafiria hati ya kimataifa alizopewa na Kwame Nkurumah wa Ghana, pamoja na Gamel Abdel Nasser wa Misri.
Odinga alihitaji hati hiyo kwa kuwa baba yake alitaka amalizie masomo yake nchini Ujerumani baada ya kukatishwa masomo akiwa kidato cha pili mwaka 1962 katika Shule ya Maranda.
Katika kitabu hicho, Odinga alisema hakushangaa kunyimwa hati hiyo.
Katibu wa baba yake aitwaye Olwande K'Oduol alimpeleka kwa Ofisa Afya wa Halmashauri ya Jiji la Nairobi, Rading Omolo ambapo alipigwa chanjo ya homa ya manjano.
"Nilipopata cheti cha chanjo hiyo tulirudi nyumbani kwa K'Oduol ambapo nilikuta vijana wengine wawili Mirulo na Oudia ambao nao walikuwa wakisafiri nje kusoma, hivyo tukaungana katika safari moja," alisema Odinga katika kitabu hicho.
Alisema siku iliyofuatia waliamka mapema ili wawahi basi la kwenda Dar es Salaam ambapo walifika kituoni saa 12 asubuhi na waliondoka Nairobi saa 1:30 asubuhi kwa kutumia basi la kampuni ya Overseas Transport Company (OTC).
Wakati huo, barabara ya lami ya Nairobi ilikuwa inaishia njiapanda ya Uwanja wa Ndege wa Jomo Kenyatta na kuanzia hapo hadi Namanga barabara ilikuwa ni mbaya, anaeeleza Odinga.
"Utaratibu wa kuvuka mpaka ulikuwa rahisi, tulipata kifungua kinywa katika eneo hilo na kuondoka baada ya muda ambapo kituo kingine kilikuwa ni Arusha. Basi hilo lilipakia abiria wengine kabla ya kufika Moshi na kupata chakula cha mchana," anasema Odinga na kuongeza;
"Tulipitia Korogwe, Handeni hadi Morogoro ambapo barabara ya lami ilianza kuonekana tena na tulifika Dar es Salaam saa 1:30 asubuhi baada ya safari ya saa 24 na tulipokelewa na Dola Osman ambaye alikuwa ni Katibu wa Katibu Mkuu wa TANU, Oscar Kambona."
Odinga anaeleza katika kitabu hicho kuwa Osman aliwapeleka hotelini na kuwaacha kwa kuwa walikuwa wachafu na wenye njaa kutokana na safari ndefu. Walioga na kubadilisha nguo kisha kupata kifungua kinywa, ndipo Osman aliporudi na kuchukua picha tatu ndogo kwa kila mmoja ambazo walitakiwa kuwa nazo.
"Haikuchukua muda mrefu kwani kabla hata hatujamaliza chakula cha mchana, Osman alirudi na hati zetu za kusafiria akitueleza kuwa kila kitu kimeshakamilika;
"Siku moja kabla ya kuondoka kwetu, Osman alituchukua saa 3 asubuhi na kutupeleka ofisini kwa Waziri Mkuu, Mwalimu Julius Nyerere ambapo Mwalimu alifurahi sana kutuona na kunieleza kuwa Jaramongi ni rafiki yake wa karibu, pia alitueleza kuhusu safari yake ya Kisumu mwaka uliopita alipohudhuria mkutano wa Pan African," anasema.
Baada ya hayo waliingia kwenye gari la Nyerere hadi nyumbani kwake ambapo walipata chakula cha mchana, kisha Mwalimu aliwatakia safari njema na masomo mema.

No comments:

COMMENTS

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...