facebook likes

Thursday, August 29, 2013

WABUNGE WA TANZANIA NAO WASUSIA KIKAO CHA BUNGE LA AFRIKA MASHARIKI

Kikao cha Bunge la Afrika Mashariki (EALA), jana kilivunjika kwa mara ya pili baada ya Wabunge wa Tanzania, kutoka ndani ya ukumbi wakipinga kanuni kuvunjwa juzi. 
SOMA ZAIDI.............Baada ya wabunge wa Tanzania kutoka nje, Spika wa Bunge hilo, Margareth Zziwa aliahirisha Bunge kwa dakika 15 ili kuweka mambo sawa, lakini jitihada za kuwashawishi ziligonga mwamba na kuamua kuahirisha Bunge hadi leo.
 
Hata hivyo, Mbunge wa Tanzania, Makongoro Nyerere hakuungana na wenzake kugoma kwani alibakia ukumbini na kuungana na wabunge 32 wa Burundi, Kenya, Uganda na Rwanda.
 
Awali, Mbunge Abdullah Ali Hassan Mwinyi alitoa msimamo wa wabunge wa Tanzania kuwa walitoka, kupinga kitendo cha wabunge wengine kudharau kiti cha Spika juzi na kutoka nje ili kushinikiza hoja yao.
 
Mwinyi alisema ili kushinikiza kuheshimiwa kiti cha Spika, wameamua kutoka nje ya ukumbi huo kwa kuonyesha hawaungi mkono, tabia ya baadhi ya wabunge kushinikiza hoja zao, kujadiliwa na Bunge hata kwa kukiuka kanuni na taratibu.
 
“Jana(juzi) ilikuwa ni mara ya pili wenzetu, kudharau kiti cha Spika na kutaka kutoa hoja na kujadiliwa bila kufuata kanuni, sasa tumeona ni vizuri na sisi kwa kupinga kuvunjwa kanuni, tutoke ili kuonyesha tunapinga mchezo huu,” alisema Mwinyi.
 
Mwinyi alisema kitendo cha wabunge wenzao kutoka nje ya ukumbi kwa kukataliwa kuvunja taratibu, kinadhalilisha kiti cha Spika na hata wabunge wenyewe.
 
Mbunge mwingine wa Tanzania, Twaha Taslima alisema kanuni zipo wazi kuwa kama mbunge ana hoja na kutaka Bunge lijadili mambo ambayo si ya dharura ni lazima aiwasilishe saa 24 kabla kwa Spika.
 
“Sasa jana(juzi), Mbunge wa Kenya, Peter Mathuki alitaka hoja yake ya kutaka utaratibu wa kufanyika bunge kwa mzunguko ijadiliwe kitu ambacho hakikuwa sahihi,” alisema Taslima.
 
Muthuki, juzi aliungwa mkono na nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), isipokuwa Tanzania.
Jana aliwasilisha hoja hiyo kwa kufuata utaratibu lakini haikujadiliwa baada ya wabunge wa Tanzania kutoka nje.
 
Katika hoja hiyo, msimamo wa wabunge wa Tanzania na Kamati ya Uongozi ya Bunge ni kuwa vikao vyote vifanyike katika ukumbi wa Bunge, Arusha baada ya kukamilika. 
Wabunge wa Tanzania ambao jana walitoka ni Shyrose Bhanji, Profesa Nderakindo Kessy na Taslima. Wabunge wanne hawakuwapo.
 
Kwa mujibu wa kanuni za Bunge hilo, kama wabunge watatu wa nchi moja, wakitoka nje kupinga jambo lolote basi kikao kinaahirishwa kwa dakika 15 na wasiporejea bunge linaahirishwa.
 
Akizungumzia mgogoro huo, Ofisa Habari wa EALA, Bobi Odiko alisema kilichotokea jana si ukiukwaji wa taratibu na kuongeza kuwa ana imani mambo yatakuwa sawa na vikao vitaendelea leo kwa amani.

source-Mwananch
i

No comments:

COMMENTS

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...