facebook likes

Tuesday, September 10, 2013

Wanaswa na dawa za kulevya Ethiopia


Kamishna wa Kupambana na Madawa ya Kulevya nchini, Godfrey Nzowa akizihesabu kete 43 za dawa za kulevya aina ya Heroin jana, zilizokamatwa katika  Uwanja wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere, jijini Dar es Salaam, juzi usiku ambapo zilikuwa zikisafirishwa kwenda nchini Japan. 
 Dar es Salaam. Mshambuliaji wa nyota wa zamani wa timu ya soka ya Simba na Taifa, Joseph Kaniki ‘Golota’ na bondia Mkwanda Matumla wanashikiliwa huku Addis Ababa, Ethiopia wakituhumiwa kusafirisha dawa za kulevya.
SOMA ZAIDI....
Kukamatwa kwao kumezidi kuongeza idadi ya Watanzania maarufu waliotiwa mbaroni nje ya nchi katika siku za karibuni wakituhimiwa kwa makosa hayo.
Tukio hilo limetokea miezi miwili baada ya Watanzania wawili, wasanii Agnes Gerald Masogange na Melisa Edward kukamatwa kwenye Uwanja wa Oliver Tambo, Afrika Kusini wakituhumiwa kusafirisha dawa za kulevya zenye uzito wa kilo 150 na thamani ya Sh6bilioni.
Aidha, hilo limetokea baada ya meli ya mizigo ya Gold Star iliyosajiliwa nchini kukamatwa na maofisa Forodha na askari wa doria wa Italia katika Pwani ya Sicily, Bahari ya Mediterranean ikiwa na tani 30 ya dawa za kulevya aina ya bangi zenye thamani ya Pauni za Uingereza 50milioni (Sh125 bilioni).
Kaniki na Matumla walikamatwa Agosti 31, mwaka huu kwenye Uwanja wa Ndege wa Bole, Addis Ababa wakati wakijiandaa kupanda ndege ya Shirika la Ndege la Ethiopia tayari kwa safari ya kuelekea Paris, Ufaransa.
Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia, Samuel Shelukindo alithibitisha jana kwamba wanamichezo hao wanashikiliwa nchini humo na Polisi wa Kitengo cha Uchunguzi wa Makosa ya Jinai.
Wanamichezo hao wamepandishwa kizimbani katika Mahakamu Kuu ya Ethiopia iliyoko kwenye eneo la Arada, Addis Ababa kujibu tuhuma za kubeba kilo saba za dawa hizo haramu. Mkwanda anadaiwa kubeba kilo nne wakati Kaniki akidaiwa kubeba kilo tatu. Kama watapatikana na hatia, wanaweza kufungwa kifungo cha miaka tisa hadi 15.
Alisema uwezekano wa kesi ya Kaniki na Matumla kurudishwa Tanzania haupo kwa kuwa nchi hizi mbili hazina utaratibu wa kubadilishana wafungwa.
“Wameshikiliwa hapa Ethiopia kwa zaidi ya siku 10 sasa, sisi tulipigiwa simu na polisi wa hapa Alhamisi iliyopita kujulishwa kwamba kuna Watanzania wawili wameshikiliwa kwa tuhuma za kukutwa na dawa za kulevya, tulipokwenda tukamkuta ni Kaniki na Matumla,” alisema Shelukindo.
“Wao wenyewe wanaeleza kwamba walipitia Mombasa na huo mzigo walipewa na mtu mmoja. Lakini Kaniki yeye anajitetea kwamba huyo aliyewapa huo mzigo pale Mombasa anajuana vizuri na Mkwanda. “Kwa hiyo alichofanya yeye ni kuubeba tu. Walikuwa wapitie hapa Addis wakashuke Paris, Ufaransa ndipo warudi Sweden kwa njia zao wanazojua wenyewe. Walipofika hapa Mkwanda alifanikiwa kupenya akapanda ndege lakini Kaniki akanaswa na mbwa ndipo akajitetea kwa polisi kwamba lile begi lilikuwa lake lakini mizigo mingine ilikuwa ya Mkwanda.
“Ndipo hapo sasa Mkwanda akashushwa kwenye ndege wakashikiliwa na Jumatatu ya wiki iliyopita wakapandishwa kwenye Mahakama ya hapa kutajiwa kesi yao lakini hawakupewa nafasi ya kujitetea. Kesi itatajwa tena Jumanne (leo) na Jumatano (kesho) na uchunguzi wa polisi bado unaendelea.”
Wanamichezo hao walidai kwamba walikabidhiwa mizigo hiyo kwenye Uwanja wa Ndege wa Mombasa walipokuwa wakikabidhiwa pasi za kupandia ndege baada ya kupita sehemu zote za ukaguzi.





No comments:

COMMENTS

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...